Saturday, December 2, 2017

Mawingu Tz

Lile Sakata La Kususia Vyumba::Kaseke, Kenny Ally, Singida United Wayamaliza "Kiume"

Uongozi wa Singida United umekubali yaishe na kuamua kuwarejesha kikosini kiungo mshambuliaji wao, Deus Kaseke pamoja na kiungo mkabaji Kenny Ally.

Uamuzi huo umetolewa ikiwa ni siku chache tangu uongozi wa Singida United kumsimamisha Kaseke na kiungo mwingine Kenny Ally kwa kile kilichodaiwa utovu wa nidhamu.

Kaseke amejiunga na Singida United msimu huu wa Ligi Kuu Bara akitokea Yanga baada ya mkataba wake kumalizika msimu uliopita.

Kaseke alisema wamefikia makubaliano mazuri na uongozi katika kutimiza mahitaji yao, hivyo ataonekana akiwa anaichezea timu hiyo katika mechi zijazo.
Kaseke alisema, anatarajia kujiunga na timu hiyo wikiendi hii kabla ya mazoezi ya timu hiyo kuanza Jumatatu baada ya mapumziko ya wiki moja waliyopewa wachezaji wote.

 “Sina kinyongo, narejea katika timu na nguvu mpya ya kupambana, nitajiunga nao kati ya kesho (leo) Jumamosi au (kesho) Jumapili na Jumatatu tutaanza mazoezi.

“Tumefikia muafaka na uongozi na wameniambia nirejee kwenye timu kwa ajili ya mechi zijazo za ligi kuu,” alisema Kaseke anayemudu pia kucheza nafasi ya kiungo mkabaji.

SOURCE: CHAMPIONI

Tupe Maoni Yako