Tuesday, December 12, 2017

Mawingu Tz

Hii Ni Taarifa Njema Kwa Wanayanga Kuhusu Uwanja Wa Kaunda

Uongozi wa Klabu ya Yanga umefunguka kuwa unakumbana na changamoto nyingi katika kuendeleza ukarabati wa uwanja wake wa Kaunda kutokana na gharama kubwa za vifusi pamoja na mvua kuendelea kunyesha hivi sasa, hivyo kusababisha kuwa katika wakati mgumu.


Yanga ipo katika mchakato wa kutengeneza uwanja wake wa Kaunda uliopo makao makuu ya klabu hiyo yaliyopo maeneo ya Jangwani jijini Dar es Salaam, ili uweze kutumika kwa ajili ya mazoezi kwa wachezaji.

Katibu Mkuu wa Yanga, Boniface Mkwasa, alisema zoezi la ujenzi wa uwanja wao limeonekana kuwa gumu kutokana na changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo na kudai kuwa wanajitahidi kuhakikisha wanazipatia ufumbuzi ili kufanikisha zoezi hilo kwa wakati.

“Kuna changamoto nyingi ambazo tunakumbana nazo katika maendeleo ya ujenzi wa uwanja, vifusi vimekuwa havipatikani, tumekuwa tukisaka kila mahali na pale tunapovipata inakuwa ni gharama kubwa kuvifikisha hapa klabuni.

“Mvua pia imekuwa kikwazo kikubwa kufanikisha zoezi letu hilo la upatikanaji wa vifusi, lengo letu ni kuhakikisha tunafanikiwa kumaliza ndani ya wakati lakini changamoto hizo zinatukwamisha, tutaendelea kupambana nazo.


“Kuhusu gharama ambazo tutazitumia kutengeneza uwanja hadi sasa bado hatujazifahamu, kwani mchakato wa awali uliopo ni kujaza vifusi kisha hapo baadaye ndiyo tutajua tutatengeneza uwanja wa aina gani na kufahamu gharama halisi, tuna mainjinia wengi pamoja na wadau mbalimbali ambao wataweza kufanya mchakato huo wa mchanganuo wa ujenzi wa uwanja kwa ujumla,” alisema Mkwasa.


Tupe Maoni Yako