Monday, January 8, 2018

Mawingu Tz

Masikini Aveva; Hali Yake Si Nzuri, Juhudi Zafanyika Kumhamishia Muhimbili Kwa Matibabu Zaidi


Masikini Mwenyekiti wa Simba! Maana hali ya afya ya Rais wa Simba, Evans Aveva bado siyo nzuri kwani jana jioni ndugu na marafiki wa karibu walikuwa kwenye mipango ya kumhamishia Hospitali ya Muhimbili.

Aveva jana alikimbizwa kwenye Hospitali ya Temeke, Dar baada ya hali yake kubadilika akiwa mahabusu kwenye Gereza la Keko.

Aveva na makamu wake, Geofrey Nyange ‘Kaburu’, wanakabiliwa na tuhuma za kughushi nyaraka za klabu hiyo na kutakatisha dola 300,000 (zaidi ya Sh 650 milioni) na wamekuwa rumande tangu Juni 29, mwaka jana.

Taarifa zinaeleza, familia na marafiki wa Aveva walikuwa na mazungumzo na Jeshi la Magereza kwa ajili ya kuomba uhamisho wa hospitali kutokana na aina ya matibabu anayoyapata Hospitali ya Temeke.

Mtoa taarifa huyo alisema, rais huyo anahitaji kupatiwa matibabu mazuri yatakayoendana na ugonjwa ambao ni siri ili apate nafuu arejee katika hali yake ya kawaida.

“Aveva jana (juzi) asubuhi hali yake ilibadilika na kusababisha akimbizwe kwenye Hospitali ya Temeke kwa ajili ya kupata matibabu ya afya yake.

“Lakini wakati akiendelea na matibabu Temeke, baadhi ya ndugu na marafiki wamejaribu kuliomba Jeshi la Magereza kwa ajili ya kupata ruhusa ya kumhamishia Hospitali ya Muhimbili kwa ajili ya kupata matibabu mazuri,” alisema mtoa taarifa huyo.


Alipotafutwa Kaimu Makamu wa Rais wa timu hiyo, Idd Kajuna kuzungumzia hilo, simu yake ya mkononi haikuwa ikipokelewa, lakini alipotafutwa Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa timu hiyo, Hajji Manara kuzungumzia hIlo, alisema: “Mimi nipo Zanzibar sifahamu chochote kuhusiana na taarifa hizo, naomba waulize watu waliopo Dar.”

SOURCE: CHAMPIONI

Tupe Maoni Yako